SIKU kadhaa baada ya Shirikisho la Soka Tanzania kuwakutanisha Ramadhan Singano ‘Messi’  na Simba katika kikao cha pamoja kujadili utata wa mkataba na pande zote mbili kufikia makubaliano ya kuifuta mikataba yote na kuanza mazungumza mapya, Mwanasheria Alex Mgongolwa ametumia dakika chache kueleza sakata hilo.
Kumbuka Singano anasema alisaini mkataba wa miaka miwili unaoisha Julai 2015 wakati Simba wanadai nyota wao huyo alisaini miaka mitatu na mkataba wake utaisha Julai 2016.
Kutokana na utata huo, TFF iliamua kuwakutanisha na kufanya mazungumzo ya pamoja na kufuta mikabata yote, lakini ilishindwa kubainisha mkataba upi ni halali na nani ameghushi.
Hapo ndipo hoja ya Msingi imesimama na watu wengi wanataka kujua nani alihusika kughushi mkataba huo?

Katika kuendelea kupata ufafanuzi, Kituo cha Azam TV kilifika ofsini kwa Mwanasheria Alex Mgongolwa ambaye amewahi kuwa mwenyekiti wa kamati ya Sheria na hadhi za wachezaji TFF ikitaka kujua kisheria suala hili liko vipi .

Mgongolwa ametoa maelezo haya ya kisheria, tumia muda wako kuyasoma;

“Yale yalikuwa ni maoni na ushauri kutoka sekretarieti ya TFF, ukiangalia muundo wa katiba ya TFF imeainisha kwamba vitakuwepo vyombo au kamati zitazokuwa na majukumu ya kufanya maamuzi katika masuala  mbalimbali yanayojitokeza katika kazi za Shirikisho.
Ipo kamati ya ufundi ambayo hushughulikia masuala yote ya ufundi, ipo kamati ya mashindano, ipo Bodi ya ligi, ipo kamati ya Sheria.
Suala la Ramadhan Singano 'Messi' ni suala ambalo lina muonjo wa moja kwa moja wa kisheria. TFF ina kamati ya sheria ambayo wajibu wake mkubwa ni kupitisha usajili na kuangalia masuala yote ya kisheria ikiwemo katiba, kanuni na taratibu mbalimbali za TFF.
Kwa namna ambavyo maoni ya TFF yametoka,  yanaweza kutumika kama ushahidi endapo upande mmoja haujaridhika na ushauri ule waliopewa na kupeleka kamati inayohusika ambayo ni kamati ya Sheria.
Ukiangalia ule ushauri au maoni, kwanza TFF inakiri kwamba kwa wakati huu, Messi hana mkataba na Simba, kama angekuwa na mkataba, TFF ingesema bayana kwamba Shauri hili limeletwa kabla ya wakati kwasababu wewe mchezaji una mkataba na klabu yako. 

Kipindi ambacho una mkataba na klabu yako kinachohitajika kufanyika ni utekelezaji wa yale mliyokubaliana, lakini mkataba huo unapokwisha ndipo kuna haja ya kuwa na makubaliano ya mkataba mpya.
Zipo kanuni mbalimbali zinazotawala wakati wa uingiaji wa mkataba, kanuni kubwa ni ridhaa ya pande zote mbili, hata wakishauriwa kama walivyoshauriwa, sheria inazuia watu kulazimishwa kuingia kwenye makubaliano.
Kwahiyo bado kanuni ile ya ridhaa itatumika, ikitokea kwamba pande hizi mbili hazijakubaliana, basi hakuna kinachofanyika kulazimisha upande mmoja uje katika makubaliano.
Kwa mujibu wa Sheria za CAF za mashindano, hata kule kughushi ambako kumefanyika kwa bahati mbaya, yaani bila kujua, bila kuwa na dhamira  kuna adhabu yake.  Unakumbuka suala la Nurdin Bakari, ilidhihirika na CAF kwamba, kweli Tanzania tulitoa taarifa za mchezaji ambazo si sahihi bila kudhamiria, adhabu iliyofuata pale ni kutolewa katika mashindano.
Unajua dhana ya kughushi inajitokeza pale ambapo mmoja anataka kupata faida kwa jambo ambalo katika hali ya kawaida lisingeweza kumpa faida ile anayoitaka, kwa mfano, mkataba wa mchezaji unaisha mwaka huu na wewe usingepende uingie tena kwenye makubaliano ya hela nyingine hapo unaweza kughushi, lakini ni tabia ambayo haifai, ila ipo na sheria inakataza kufanya hivyo.
Haya yanayotokea ni bahati mbaya sana kwamba yanatokea kwenye familia ya mpira ambayo inaheshimu utaratibu wake, angalia michezo inapochezwa wakati wote kuna bendera ya ‘Fair Play’,  mchezo wa kiungwana. Kama mkataba wa mchezaji umekwisha kaeni naye tena, muingie mkataba mwingine, ukiisha na bado mna mapenzi naye mnazungumza tena”.

Haya ni maelezo ya Mwanasheria Alex Mgongolwa…….

AddThis

 
Top